Home BUSINESS HALMASHAURI YA WILAYA MBINGA YAKABIDHI KIWANDA CHA MATOFALI KWA KIKUNDI CHA VIJANA

HALMASHAURI YA WILAYA MBINGA YAKABIDHI KIWANDA CHA MATOFALI KWA KIKUNDI CHA VIJANA

 

Mkuu wa Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma Cosmas Nshenye wa tatu kulia,akikabidhi mashine ya kufyatua tofali kwa mwenyekiti wa kikundi cha Chipukizi Kigonsera Keneth Mbena kushoto iliyotolewa na Halmashauri ya wilaya ya Mbinga ikiwa ni mkopo wenye masharti nafuu ili iweze kusaidia wananchama wa kikundi hicho waweze kujitegemea na kujinasua na umaskini,kulia Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Juma Mnwele na wa pili kulia Mwenyekiti wa Halmashauri Desdelius Haule.
Afisa Mipango miji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Frank Kaseka aliyeshika fimbo akimuonesha Mkuu wa wilaya ya Mbinga Cosmas Nshenye kulia, Ramani ya majengo ya Hospitali ya Halmashauri inayojengwa katika kijiji cha Kigonsera kata ya Kigonsera ambapo itakapokamilika inatarajia kuhudumia zaidi  ya wakazi  232,000,katikati Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Juma Mnwele.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Cosmas Nshenye kulia,akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga Juma Mnwele alipotembelea ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri hiyo.
Picha na Muhidin Amri.

Na: Muhidin Amri, MBINGA

Halmshauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma,katika kipindi cha miaka miwili imetoa shilingi  344,049,155.07  kwa vikundi 17 vya vijana,wanawake na walemavu  ili kuvijengea uwezo  kiuchumi.

Afisa Maendeleo ya jamii wa Halmashauri hiyo Pascal Ndunguru amesema hayo jana wakati wa  kukabidhi kiwanda  cha kufyatua tofali kwa kikundi cha vijana cha Chipukizi Kigonsera ikiwa ni Utekelezaji wa sheria na maagizo ya serikali ya kutenga asilimia kumi ya mapato ya ndani ya Halmashauri.

Kwa mujibu wa Ndunguru, tangu mpango huo ulipoanza kutekelezwa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga imeshatoa zaidi ya shilingi 560,000,000 ambazo zimekwenda kwenye vikundi mbalimbali na kwa wananchi.
Alisema,pamoja na kutekeleza maelekezo ya Serikali ya kukopesha asilimia kumi,Halmashauri ya wilaya Mbinga iliamua kujielekeza zaidi katika falsafa ya kukopesha mitaji na vitendea kazi  kwa lengo la ukuzaji na uendelezaji wa viwanda.
Ndunguru alisema, kiwanda hicho kina seti moja ya mashine ya kuchanganya zege,mashine ya kuchanganya mchanganyiko wa mchanga na saruji vyote vikiwa na thamani  ya shilingi milioni 17,549,999.07.

Alisema, kiwanda hicho cha vijana kina uwezo wa kufyatua tofali za kisasa,ngumu na zenye ubora unaokidhi mahitaji ya majenzi ya Serikali na kwa siku kina uwezo wa kufyatua tofali 2000 na vijana  hao wamepatiwa  mafunzo ya kuendesha mitambo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Juma Mnwele alisema pamoja na seti  ya mashine,Halmashauri imetoa shilingi milioni  4,680,000 kwa kikundi hicho kama mtaji na hivyo kufanya mkopo wote kufikia shilingi milioni 22,229,999.
Alisema, kwa kuanzia kiwanda  kitaanza kufyatua tofali kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Halmashauri ya wilaya kwa makubaliano ya kufyatua tofali 28,000 na hivyo  kujipatia kipato moja kwa moja.
Aidha alisema, mtambo wa kukoroga zege utakodishwa na Halmashauri kwa makubaliano ya ujirani mwema  kwa pande zote mbili na vijana hao wataendelea kupata kazi nyingi za serikali na watu binafsi ikiwemo tofali kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya wilaya.

Mwenyekiti wa kikundi Kenneth Mbena alisema,kikundi kilifikia uamuzi wa kuomba mkopo wa mashine ya kufyatua tofali hasa baada ya kuona kuna fursa ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri  pamoja na jengo la Utawala.
Hata hivyo alisema, matumaini yao kuendelea kupata kazi hata baada ya miradi  hiyo miwili kukamilika kwani wamejipanga kuhakikisha wanazalisha tofali bora zitakazotumika kwenye miradi ya ujenzi.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Cosmas Nshenye ameipongeza Halmashauri ya wilaya ya Mbinga kwa kutoa fedha za kujenga kiwanda hicho ambacho kitasaidia wananchi kupata tofali bora kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za makazi na ofisi za serikali.

Alisema, kuanzishwa kwa kiwanda hicho kinakwenda kufungua fursa mpya kwa wakazi wa Mbinga kuanza kujenga nyumba kwa kutumia tofali za saruji na mchanga badala ya mazoea ya kujenga kwa kutumia tofali za udongo.

Amewaasa wana kikundi hicho kuhakikisha wanazalisha tofali zenye ubora ili waweze kujitangaza na kupata soko kubwa la ndani nan je ya wilaya ya Mbinga.
MWISH

Previous articleKUTOKA MEZA YA MAGAZETI ASUBUHI YA LEO J.TATU JUNI 7-2021
Next articleTANZANIA NA KOREA KUSINI WATIA SAINI MAENEO YA USHIRIKIANO

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here