Home LOCAL HALMASHAURI YA MALINYI KUWAKAMATA WAVAMIZI BONDE LA MAJI LA MWALIMU NYERERE.

HALMASHAURI YA MALINYI KUWAKAMATA WAVAMIZI BONDE LA MAJI LA MWALIMU NYERERE.

Na: Mwandishi Wetu Malinyi.

HAlMASHAURI  ya Wilaya ya Malinyi Mkoani Morogoro imesema, imeanza harakati za kuwakamata waliovamia hifadhi ya Bonde la Maji la Mwalimu Nyerere lililopo Wilayani humo kwa kufanya maendeleo ya kilimo na ufugaji.

Imesema  kuwa bonde hilo ambalo ni hifadhi ya kupeleka maji katika Bwawa la kufua umeme la Mwalimu Nyerere, Rufiji, hatua hizo kali zimeanza kuchukuliwa na tayari baadhi ya watu kadhaa wameshakamatwa na wanahojiwa na maofisa wa hifadhi hiyo.

Akizungumza hatua hiyo hivi karibuni  Wilayani humo Mkuu wa wilaya  hiyo Mathayo Masele alisema, kifungu kidogo (1c) cha sheria namba (5) kwa wanaovamia hifadhi ya wanyama pori lazima wakamatwe

Masele amesema kwa sasa takriban wananchi  nane (8) wameshakamatwa na wapo rokapu kwa mahojiano na msako wa kuwasaka  bado unaendelea lengo ikuwakamata wote wanaofanya uharibifu huo.

Amefafanua kuwa katika msako huo  Trekta 10 zimekamatwa na  zimeshikiliwa katika kituo cha polisi Mtimbira huku trekta nyingine moja ambayo ni ya mwanasiasa mmoja hapa nchini nayo  imeshikiliwa katika kituo cha polisi Ifakara.

“Nikweli kwamba kuna trekta kumi zinashikiliwa na zimehifadhiwa katika vituo viwili vya polisi, moja ipo katika kituo cha polisi Ifakara, trekta hiyo ni ya mwanasia mmoja mkubwa hapa nchini na zingine zimeshikiliwa katika kituo cha polisi Mtimbira wilayani hapa”. Amesema mkuu wa wilaya huyo Masele.

Ameongeza kuwa , wavamizi wengi wanaovamia hifadhi hiyo sio wananchi wa Malinyi, ni watu ambao wanatoka katika mikoa ya Dar es Salaam na mkoa wa Morogoro ambao wanashawishiwa na madalali wachwara wasiolitakia taifa maendeleo.

Akizungumzia  namna  uvamizi huo unavyofanyika alisema watu wanakimbilia katika bonde hilo kwa  kile walichodai ni rutuba na kuwepo kwa nyasi chache ambapo hutumia kemikali kwa ajili ya kuangamiza nyasi hizo na kisha kumwaga mpunga.

Ameongeza kwa baadhi ya viongozi pamoja na wananchi wamekuwa wakikaidi maagizo ya serikali, kwani tangazo la kukatazwa kufanya maendeleo ya kilimo katika hifadhi hiyo la bonde lilitolewa mapema na walielezwa kwamba  linachangia 65% ya maji kwenda kwenye bwawa la Mwalimu Nyerere.

Masele amesema  kuwa bonde hilo lilianzishwa mwaka 1952 ambalo lenye ukubwa wa kilometa za mraba 6500 kwa huruma ya serikali wananchi walipewa eneo la kilometa 4300 kwa ajili ya kufanya maendeleo ya kilimo.

Kwa upande wa wananchi wa maeneo ya Mtimbira, Itete na Songwa, walisema awali walitahadharishwa kuacha kufanya maendeleo ya kilimo kwa kuitisha kikao Novemba 2020 lakini  hawakujua kama ni kitu gani kitakujakutokea mwisho wa siku.

Hata hivyo wananchi wa Kata ya Mtimbira na Itete Wilayani humo wamemtaka  Rais Samia Suluhu Hassan kuingilia kati mgogoro huo Kwa madai  kuwa hawatendewi haki kwani wanakamatwa bila makosa.

Wananchi hao wanadai  mgogoro huo unarudisha nyuma maendeleo, kwani asilimia kubwa ya vijiji ndani ya wilaya hiyo wanategemea kilimo cha mpunga nakwamba kwao ndio zao kuu la biashara wilayani humo.

  Mwisho

Previous articleMISS DODOMA KUMENOGA.
Next articleWATU WENYE MATATIZO YA UGUMBA WAIOMBA JAMII ISIWATENGE.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here