Home LOCAL VYAMA VYA SIASA VYAONESHA USHIRIKIANO UBORESHAJI DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA...

VYAMA VYA SIASA VYAONESHA USHIRIKIANO UBORESHAJI DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA TABORA

Mkazi wa Kata ya Ng’ambo aliyefika katika Kituo cha Kizigo Mzee Juma Rai  Juya, akionesha kadi yake ya mpiga kura mara baada ya kukamilisha taratibu za kuboresha taarifa zake kwenye daftari la wapiga kura na Kukabidhiwa kadi yake mpya.

Afisa Mtendaji wa kata  na  Mwandikishaji Msaidizi Kata ya Ng’ambo, Rehema Midelo akizungumza na mwandishi wetu katika kituo cha Masempele kata ya Ng’ambo mjini Tabora wakati akielezea namna zoezi hilo linavyoenda kwa ufanisi mkubwa.

Wakala wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Kituo Cha Kaze Shule ya Sekondari, Bw. Brayson Dickson akielezea namna zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wazpiga kura linavyoendelea katika kituo cha Shule ya Sekondari Kaze mjini Tabora.

Bi Leila Muhaji Kaimu Mkurugenzi Masidizi Habari kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi kulia akifuatilia zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika kituo cha Kizigo kata ya Ng’ambo mkoani Tabora.

Vyama vya Siasa pamoja na Wakazi wa Kata ya Ng’ambo, Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, Mkoa wa Tabora wameonesha ushirikiano mkubwa wa kushiriki katika zoezi la uboreshaji wa majaribio wa daftari la kudumu la wapiga kura linaloendelea katika Kata ya Ng’ambo.

Akifanya mahojiano na Mwandishi Wetu, Afisa Mtendaji na  Mwandikishaji Msaidizi Kata ya Ng’ambo, Rehema Midelo, amesema kuwa mwitikio ni mkubwa na wananchi wameendelea kujitokeza kujiandikisha katika zoezi la uboreshajia wa majaribio wa daftari la kudumu la wapiga kura.

Bi. Midelo amesema kuwa katika zoezi hilo mpaka Novemba 26, 2023 kuna wapiga wengi wamejitokeza katika uboreshaji wa  daftari la kudumu la wapiga kura.

“Wananchi wa Kata ya Ng’ambo wana hamasa kubwa katika ushiriki wa shughuli za kijamii na maendeleo ikiwemo zoezi  hili la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura ambalo baadaye linawapa uhalali wa kushiriki kuchagua viongozi wao wakati wa uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani” amesema.

Amefafanua kuwa Kata ya Ng’ambo kuna mitaa 10, huku mtaa wa Kizigo ukiwa na  idadi kubwa ya watu ambao wanajitokeza  katika zoezi la uboreshajia wa  daftari la kudumu la wapiga kura, Hii imepelekea Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuongeza mashine mbili zaidi za BVR Kit na kufikisha tatu katika kituo hicho hata hivyo inapofika jioni bado kuna watu wanabaki ambapo wanaelekezwa kurudi kituoni kesho yake ili kumalizia taratibu zilizobaki.

“Mtaa huu kuna wapiga kura wengi, lakini kuna changamoto ya baadhi ya watu kutoka kata, jirani wamekuwa wakijiandikisha na tukiwabaini tunawapa elimu na kuwarudisha katika maeneo yao na kuwaelimisha kuwa  zoezi bado halijaanza rasmi  na likianza watatangaziwa” amesema.

Wakala wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Kituo Cha Kaze Shule ya Sekondari, Bw. Brayson Dickson, amesema kuwa wanachama wa CCM wamehamasika  kwa asilimia kubwa na walio wengi ni vijana ambao pamoja na kufanya mikutano ya kuwahamasisha lakini tulitenga muda wa kuwafuata vijana katika vijiwe vyao na kuwaelimisha kuhusu zoezi hili ndiyo maana unaona mwitikio ni mkubwa sana kwa vijana.

“Baada ya kutoa elimu mwitikio ni mkubwa sana, na kituo hiki hakuna changamoto yoyote, tuendelee kutoa elimu na kuhamasisha wananchi pamoja viongozi ili tuweze kufikia malengo kwa muda uliobaki,” amesema  Dickson. 

Wakala wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA)  katika kituo cha Kizigo  Jumanne Kishimba,  amesema kuwa zoezi la uboreshaji wa  daftari la kudumu la wapiga linakwenda vizuri.

“Hamasa inakwenda vizuri, hakuna shida, sisi CHADEMA tumehamasisha wanachama wetu kwa kuwapigia simu pamoja na kutembea nyumba hadi nyumba kwa ajili ya kujiandikisha,” amesema.

Naye Mkazi wa Kata ya Ng’ambo aliyefika katika Kituo cha Kizigo Mzee Juma Rai  Juya, amesema kuwa zoezi linakwenda vizuri na kila mtu anayefika anapata huduma kwa wakati.

“Nimefika hapa kituoni wakaniuliza taarifa zangu na kujaza fomu za uboreshaji wa daftari, nikapigwa picha, pia nikachukuliwa alama za vidole kisha nikapewa kadi yangu mpya ya kisasa ya kupigia kura, naishukuru serikali kwa utaratibu huu mzuri wa kuboresha taarifa na nitaitunza kadi yangu mpaka uzeeni” amesema.

Previous articleBRELA YATAKIWA KUZIFIKIA WILAYA ZOTE ARUSHA
Next articleTUME YA MIPANGO SHIRIKISHENI WANANCHI UANDAAJI DIRA YA MAENDELEO YA TAIFA 2050 – DKT. BITEKO
Hughes Dugilo is a Writer, News Producer, Video-Photographer Journalist, and Video Editor experienced for 20 years now performing in News, Documentary, Advertisements and Television Programs. Aside from all above he own and operate his Blog known as Green Waves Media TZ since 2018.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here