Home LOCAL SEKONDARI YA MWANDETI YAIOMBA SERIKALI KUSAIDIA UJENZI WA MIUNDOMBINU.

SEKONDARI YA MWANDETI YAIOMBA SERIKALI KUSAIDIA UJENZI WA MIUNDOMBINU.

Mkuu wa shule ya Sekondari Mwandet John Massawe akisoma risala ya shule katika maafali ya 15 ya kidato cha nne katika shule hiyo.

Baadhi ya wanafunzi Kati ya 280 wanahitimu katika shule ya sekondari Mwandet iliyopo Mkoani Arusha.

NA: NAMNYAK KIVUYO, ARUSHA.

Shule ya Sekondari Mwandet iliyopo wilaya ya Arumeru  halmashauri ya Arusha mkoa wa Arusha pomoja na kuwa na matokeo mazuri ya mitihani ya kitado cha sita  kwa miaka mitatu mfululizo na kupanda kila mwaka katika matokeo ya mitihani ya kidato cha nne inakabiliwa na changamoto ya  uhaba wa nyumba za walimu hali inayopelekea walimu kushindwa kutekeleza majukumu  yao ipasavyo kutokana na kukaa kilometa 13 hadi 25 kutoka eneo shule ilipo.

Akisoma risala ya shule katika mahafali ya 15 ya kidato cha nne  Mkuu wa Shule hiyo John Massawe alisema kuwa shule hiyo ina nyumba 9 za walimu huku  jumla ya walimu walioajiriwa ikiwa ni 39 na walimu wasioajiriwa 13 hali inayofanya mahitaji ya nyumba za kuishi walimu kuwa kubwa.

Massawe alisema kuwa  walimu wanalizimika kukaa umbali mrefu kutokana na kijiji na kata iliyopo shule hiyo kutokuwa na nyumba za kupanga jambo ambalo limekuwa changamoto kwani  walimu hufika kwa kuchelewa na wakati mwingine kushindwa kufika kabisa hasa nyakati za mvua kwasababu ya ubovu wa barabara ya kutoka Kilimamoto hadi shuleni hapo.

“Tatizo hili la walimu kukaa umbali mrefu limekuwa na madhara hasa kipindi cha  mvua kwani barabara kama mnavyoona hivi sasa ni mbovu mvua zikinyesha ndio hali inakuwa mbaya zaidi na kuna siku korongo linajaa maji hata wawalimu wakijitahidi kuja wanakwama hapo kwani hakuna namna ya kuweza kuvuka upande mwingine,”Alisema Mwalimu Massawe.

Kutokana na changamoto hiyo aliiomba serikali pamoja na wadau wa elimu kuwasaidia kujenga nyumba za walimu ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwani pamoja na kuwa katika kumi bora miaka mitatu mfululizo katika matokeo ya mitihani ya kitado cha sita pia wanamatarajio ya kuondoa daraja sifuri katika matokeo ya kidato cha nne.

“Na hili la kuondoa daraja sifuri litawezekana tuu pale mazingira ya walimu yatakapokuwa mazuri kwani wataweza kufundishia na kuwaelewesha vizuri wanafunzi  pamoja na  kuwafutilia kwa ukaribu  masaa yote tofauti na hivi sasa ambapo Mwalimu anafundisha huku akiwa na mawazo ya namna gani ataweza kurudi anakoishi,” Alisema.

Sambamba na hayo pia alieleza changamoto nyingine ni pamoja na shule kuingilika pande zote kutokana na kutokuwa na uzio jambo linalohatarisha usalama wa wanafunzi pamoja na mali za shule ambapo hivi karibuni mnamo tarehe 19 Septemba Bweni la wasichana wa kidato cha kwanza liliungua moto na hadi hivi sasa chanzo cha moto huo hakijajulilikana.

“Pamoja na kwamba Bweni hilo limeshakarabatiwa lakini chanzo hatukijui ambapo tukipata uzio hii itasaidia kupunguza uhalifu wa watu wachache wa nje  wasio na mapenzi mema na shule kwani tutajua pa kuanzia lakini hivi sasa ni ngumu kwani huwezi kujua muhalifu kapita wapi,” Alieleza.

Alieleza changamoto nyingine uhaba wa wa maji ambapo malmlaka ya maji na usafi wa mazingira(AUWSA) iliwaahidi kuwapa laini moja ya maji lakini hadi sasa hawajafanyanya hivyo jambo ambalo linawafanya kuagiza maji kwa kutumia boza kila siku lakini pia maji hayo hayawatishi kutokana na matumizi yaliyopo na wingi wa wanafunzi ambapo changamoto nyingine ni kutokuwepo kwa jengo la utawala hali inayowalazimu walimu kutumia madarasa kama ofisi.

Kwa upande wake Mwamvita Okeng’o mwakilishi wa afisa elimu mkoa wa Arusha ambaye pia ni Afisa michezo wa mkoa alisema kuwa  serikali inafahamu mchango mkubwa unatolewa na Mwandet katika kuwahudumia wanafunzi na kuhakikisha wanapata elimu bora  na pia wanafahamu mikakati waliyonayo katika kuinua kiwango cha elimu hapa nchini hivyo atazifikisha changamoto hizo sehemu husika.

Pia Bi Okeng’o aliwasihi wanafunzi 280 wanaohitimu katika shule hiyo kila mmoja kuhakikisha anakuwepo kati ya watakaofaulu  na hiyo itasaidia kunifanya Mwandet ipige hatua zaidi pamoja na kuzipa shule za kata heshima kubwa pamoja na kuwasihi wazazi kushirikiana bega kwa bega na hiyo.

“Kuna tatizo la utoro hasa kwa wanaoishi nje ya shule wazazi ninaomba mjisikie vibaya pale mtoto wako anapokaa siku mbili tatu bila kufika shule kwasababu anakosa mengi na ndio hawa wanakuja kufeli kwa kutohudhuria katika vipindi ipasavyo, mzazi inatakiwa ujiuliza sifa nzuri waliyonayo Mwandet mtoto wako anachangia au anaharibu,” Alisema Bi Okeng’o.

Hata hivyo shule hiyo kwa mwaka 2019 katika matokeo ya kidato cha sita ilishika nafasi ya nne kitaifa, 2020 nafasi ya 9 na 2021 nafasi ya 7 ambapo kwa kidato cha nne imeendelea kupunguza daraja sifuri ambapo kwa mwaka 2019 kulikuwa na sifuri 36 na mwaka 2020 zimepungua na kufikia 12.

Previous articleKUTOKA MAGAZETINI ASUBUHI YA LEO J.PILI OCTOBA 3-2021.
Next articleSERIKALI YAWEKA MKAKATI KUENDELEA KUMLINDA MKULIMA, YATOA MILIONI 700 UJENZI SKIMU YA USENSE MKOANI KATAVI
Hughes Dugilo is a Writer, News Producer, Video-Photographer Journalist, and Video Editor experienced for 20 years now performing in News, Documentary, Advertisements and Television Programs. Aside from all above he own and operate his Blog known as Green Waves Media TZ since 2018.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here