Home BUSINESS RIBA YA BENKI KUU (CBR) KUBAKI ASILIMIA SITA KIPICHA CHA ROBO MWAKA

RIBA YA BENKI KUU (CBR) KUBAKI ASILIMIA SITA KIPICHA CHA ROBO MWAKA

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania(BoT), Emannuel Tutuba,akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akitoa taarifa ya kamati ya fedha  leo Oktoba 3,2024 jijini Dodoma.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania(BoT), Emannuel Tutuba,akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akitoa taarifa ya kamati ya fedha  leo Oktoba 3,2024 jijini Dodoma.

 Waandishi wa habari wakimsikiliza Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania(BoT), Emannuel Tutuba, wakati akitoa taarifa ya kamati ya fedha  leo Oktoba 3,2024 jijini Dodoma.

 

Waandishi wa habari wakimsikiliza Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania(BoT), Emannuel Tutuba, wakati akitoa taarifa ya kamati ya fedha  leo Oktoba 3,2024 jijini Dodoma.

Na; Alex Sonna, Fullshangwe Blog – DODOMA

KAMATI  ya Sera ya Fedha (MPC) ya Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu ya Tanzania(BoT), imeamua Riba ya Benki Kuu (CBR) kuendelea kuwa asilimia sita kwa robo mwaka itakayoishia Disemba 2024.

Hayo yamesemwa leo Oktoba 3,2024 jijini Dodoma  na Gavana wa BoT, Emannuel Tutuba,wakati akizungumza na waandishi wa habari amesema kuwa uamuzi huo ulitokana na matarajio ya mfumuko wa bei kuendelea kuwa chini ya lengo la nchi la asilimia tano huku kamati ikitarajia uchumi kuendelea kukua kwa kasi ya kuridhisha, kuimarika kwa mazingira ya kiuchumi duniani na  nchini.

“Uchumi wa dunia unatarajiwa kuendelea kukua sambamba na kuimarika kwa mazingira ya upatikanaji fedha, kutokana na hali hii, Shirika la Fedha Duniani (IMF) na Benki ya Dunia wanakadiria uchumi wa dunia kukua kwa asilimia 3.2 na asilimia 2.6, mtawalia, mwaka 2024. Mwenendo huu unatarajiwa kuchagiza shughuli za uzalishaji hapa nchini.

“Mfumuko wa bei unatarajiwa kuendelea kupungua, ikiwa ni matokeo ya utekelezaji wa sera ya fedha inayolenga kupunguza ongezeko la ukwasi sambamba na kupungua kwa bei za bidhaa katika soko la dunia, hususan mafuta na mbolea, kutokana na hali hii, benki kuu katika nchi nyingi zinatarajiwa kupunguza au kutokubadili riba zao za sera ya fedha,” amesema Tutuba

Aidha ameeleza kuwa , Benki kuu katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) zinatarajiwa kufuata mwenendo huu wa kisera, bei za bidhaa katika soko la dunia zimeendelea na zinatarajiwa kuendelea kuwa tulivu.

“Katika robo ya mwaka inayoishia Disemba 2024, bei za mafuta ghafi zinatarajiwa kuwa kati ya dola za Marekani 72 hadi 82 kwa pipa, kutokana na ongezeko la uzalishaji. Hali hii inatarajiwa kupunguza ongezeko la mfumuko wa bei na mahitaji ya fedha za kigeni nchini kwa kuwa bidhaa za mafuta huchangia takriban asilimia 20 ya bidhaa zote zinazoagizwa kutoka nje ya nchi,” 

Kamati pia ilitathmini utekelezaji wa sera ya fedha katika robo mwaka inayoishia Septemba 2024, pamoja na mwenendo na mwelekeo wa uchumi nchini, ilibaini kuwa utekelezaji wa sera ya fedha ulifanikiwa kuhakikisha mfumuko wa bei unabaki ndani ya lengo la asilimia tano.

Katika robo ya kwanza ya mwaka 2024, uchumi ulikua kwa asilimia 5.6, huku shughuli za ujenzi, kilimo, fedha na bima, na usafirishaji zikichangia kwa kiwango kikubwa  nchini, kwa  mujibu wa viashiria vya awali, uchumi unakadiriwa kukua kwa asilimia 5.8 na asilimia 5.6 katika robo ya pili na ya tatu ya mwaka 2024, mtawalia, na unatarajiwa kuendelea kukua katika viwango hivyo katika robo ya mwisho wa mwaka.

Ukuaji huu utachangiwa na kuendelea kuimarika kwa mazingira ya kiuchumi  nchini na duniani, kuendelea kuimarika kwa mazingira ya kiuchumi nchini kunatokana na maboresho katika biashara na uwekezaji, ikiwemo yanayoendelea kutekelezwa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo.

Uzalishaji katika shughuli za kilimo unatarajiwa kuongezeka kwa kiwango kikubwa kutokana na matumizi ya pembejeo (mbolea na mbegu bora), viwatilifu na uwekezaji katika miradi ya umwagiliaji. Vilevile, shughuli za ujenzi na usafirishaji zinatarajiwa kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi.

Vilevile uchumi wa Zanzibar ulikua kwa asilimia 6.4 katika robo ya kwanza ya mwaka 2024, ukichochewa na shughuli za usafirishaji, fedha na bima, na ujenzi. ii. Mfumuko wa bei uliendelea kuwa tulivu, ndani ya lengo la nchi na vigezo vya mtangamano wa kiuchumi katika jumuiya za kikanda.

Mfumuko wa bei ulikuwa asilimia 3 na 3.1 Julai na Agosti, mwaka huu na unatarajiwa kuwa asilimia 3.2 katika robo ya nne ya mwaka 2024. Mfumuko wa bei unatarajiwa kuendelea kuwa tulivu, ukichangiwa na kupungua kwa bei za bidhaa katika soko la dunia, upatikanaji wa chakula cha kutosha na umeme wa uhakika, pamoja na utekelezaji wa sera madhubuti za fedha na kibajeti.

Kwa upande wa Zanzibar, mfumuko wa bei ulipungua hadi kufikia asilimia 5.1 kutokana na kushuka kwa bei bidhaa za chakula na zisizo za chakula, hata hivyo, migogoro ya kisiasa Ulaya Mashariki na Mashariki ya Kati inaweza kusababisha kuvurugika kwa mnyororo wa ugavi na kupelekea kuongezeka kwa bei za bidhaa katika soko la dunia.

Pia mikopo kwa sekta binafsi imeendelea kuongezeka kwa kasi ya kuridhisha ikiwa ni takriban asilimia 17.1 kwa kipindi cha Julai hadi Septemba, mwaka huu, sawa na ukuaji uliofikiwa katika kipindi cha Aprili hadi Juni Mwak huu.

Aidha, ubora wa rasilimali za benki uliendelea kuongezeka ambapo uwiano wa mikopo chechefu ulipungua hadi asilimia 3.9 mwezi Agosti mwaka huu, asilimia 5.1 katika mwezi kama huo mwaka 2023.

“Mikopo kwa sekta binafsi inatarajiwa kuendelea kuongezeka, sambamba na kuimarika kwa uchumi wa dunia na wa hapa nchini, utekelezaji wa sera ya bajeti ulikuwa wa kuridhisha, ambapo mapato ya kodi yamevuka lengo, kufuatia kuimarika kwa usimamizi na kuongezeka ulipaji kodi kwa hiyari na Serikali imeendelea kupanga matumizi kulingana na mapato,” 

Previous articleEWURA YAELIMISHA WATU WENYE ULEMAVU MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA DAR ES SALAAM  
Next articleUAUMUZI TCRA KUFUNGIA MAUDHUI MTANDAO MCL WAISHTUA TEF
Hughes Dugilo is a Writer, News Producer, Video-Photographer Journalist, and Video Editor experienced for 20 years now performing in News, Documentary, Advertisements and Television Programs. Aside from all above he own and operate his Blog known as Green Waves Media TZ since 2018.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here