Home LOCAL TEA NA UNICEF WAFUNGUA MILANGO YA MIRADI YA ELIMU ZANZIBAR

TEA NA UNICEF WAFUNGUA MILANGO YA MIRADI YA ELIMU ZANZIBAR

Thank you for reading this post, don't forget to subscribe!

Katika kuendeleza ushirikiano na wadau wa Sekta ya Elimu nchini, Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kwa kushirikiana na Shirika la Kuhudumia Watoto (UNICEF Tanzania) wamefungua rasmi milango ya utekelezaji wa miradi ya elimu visiwani Zanzibar kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali (WEMA), kwa lengo la kuboresha miundombinu ya elimu.

Kupitia ushirikiano huo, TEA na UNICEF wametenga jumla ya shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa vyumba vya madarasa, maabara za sayansi pamoja na matundu ya vyoo katika shule 20 ambapo, shule 11 zipo kisiwani Unguja na shule 9 kisiwani Pemba.

Akizungumza wakati wa kikao kazi maalum cha kujadili utekelezaji wa miradi hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Dkt. Erasmus Kipesha alisema, utekelezaji wa mradi unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Januari na kukamilika kabla ya mwezi wa sita mwaka huu.

Dkt. Kipesha alibainisha kuwa lengo la
mradi huo ni kuwawezesha wanafunzi kusoma katika mazingira bora, salama na rafiki kwa afya zao. Aliongeza kuwa TEA ni taasisi ya Muungano hivyo utekelezaji wa miradi ya elimu Zanzibar ni sehemu ya majukumu yake ya msingi.

Aidha, alisisitiza kuwa ushirikiano
uliopo kati ya TEA na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar umekuwa nguzo muhimu ya mafanikio ya miradi mbalimbali ya elimu inayotekelezwa na ambayo
imekamilika.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Bw. Khamis Said, aliishukuru TEA kwa mchango mkubwa kwenye uboreshaji wa miundombinu ya elimu huku akieleza kuwa miradi hiyo imekuwa kichocheo cha wadau wengine kujitokeza kusaidia maendeleo kwenye sekta ya elimu.

Bw. Said aliongeza kuwa ukarabati na
ujenzi wa miundombinu hiyo umefika wakati muafaka kwani majengo mengi ya shule hizo ni ya kizamani na yako katika hali isiyoridhisha. 

Alisema kukamilika kwa miradi hiyo kutachangia kuinua kiwango cha taaluma kwani wanafunzi watapata motisha ya kusoma katika mazingira ya kisasa.

“Wizara inatoa shukrani za dhati kwa TEA kwa ushirikiano mkubwa mnaoendelea kutupatia katika kuboresha miundombinu ya elimu na tunawaahidi kusimamia utekelezaji wa miradi yote kwa ufanisi ili ilete
tija kwa maendeleo ya sekta ya elimu,” alisema Bw. Said.

 Kwa sasa TEA inaendelea kutekeleza
miradi mbalimbali ya miundombinu ya elimu Zanzibar kama taasisi ya Muungano.

Awali, jumla ya shilingi bilioni 3.2 zilitengwa kwa ajili ya ujenzi wa
miundombinu ya mafunzo ya amali ambayo utekelezaji wake bado unaendelea huku shilingi bilioni 2.5 zikitengwa kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa madarasa, maabara za sayansi na matundu ya vyoo.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Bw. Khamis Said akifafanua jambo katika kikao kazi maalum cha kujadili utekelezaji wa miradi ya elimu kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA).

  Mkurugenzi Utafutaji Rasilimali na Usimamizi wa Miradi kutoka TEA Bw. Masozi Nyirenda akisistiza jambo kuhusu utekelezaji wa miradi ya elimu inayofadhiliwa na TEA
kwa upande wa Zanzibar.

Baaddhi
ya wataalamu kutoka TEA na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar wakifuatilia
majadiliano kuhusu utekelezaji wa miradi ya uboreshaji miundombinu kwenye shule
za Unguja na Pemba unaotarajia kuanza Januari mwishoni 2026.
Muonekano
wa maabara ya sayansi itayofanyiwa ukarabati katika shule ya Sekondari Chwaka
iliyopo Wilaya ya Kati, Kusini Unguja.

  Muonekano wa vyumba vya madarasa vitakavyofanyiwa ukarabati katika shule ya Sekondari CharaweWilaya ya Kati Mkoa wa  Kusini Unguja.

Muonekano
wa matundu ya vyoo yakayojengwa upya shule ya Sekondari Kijini iliyopo Wilaya
ya Kaskazini A, Mkoa wa Kaskazini Unguja