

Arusha.
Arusha. Mashirika ya Umma yaliyofanya vizuri katika mwaka wa fedha 2023/24 yamekabidhiwa tuzo maalum na Ofisi ya Msajili wa Hazina katika hafla rasmi iliyofanyika kwenye Kikao Kazi cha Wenyeviti wa Bodi na Watendaji Wakuu wa Taasisi za Umma, kilichofunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mpango, jijini Arusha, Jumapili, Agosti 24, 2025.
Tuzo hizo zilizingatia vigezo vya kiuendeshaji kama vile ukuaji wa mapato ya ndani, udhibiti wa matumizi, kuimarisha faida (Net margin), kuboresha ukwasi (Current ratio) na rejesho la uwekezaji (ROE).
Vigezo vingine ni kupunguza utegemezi wa ruzuku ya Serikali, ufanisi katika matumizi, utekelezaji wa hoja za kikaguzi za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), uchapishaji wa taarifa za fedha, na maboresho ya utoaji huduma kwa jamii.
Taasisi zilizotunukiwa zilitangazwa chini ya makundi manne mahsusi kulingana na aina na majukumu yao.
Katika kundi la mashirika yanayofanya biashara, tuzo zilitolewa kwa mashirika yaliyoboresha mapato, faida, ukwasi na rejesho kwa mtaji wa serikali.
Washindi wa kundi hili walikuwa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Bohari ya Dawa (MSD) na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).




