Home LOCAL WIZARA YA AFYA MBIONI KUANZISHA MWONGOZO WA UFUATILIAJI KWA WALIOPONA MARBURG

WIZARA YA AFYA MBIONI KUANZISHA MWONGOZO WA UFUATILIAJI KWA WALIOPONA MARBURG

Na. Elimu ya Afya kwa Umma.

Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa Kushirikiana na Wadau wa ikiwemo Shirika la Afya Duniani(WHO) ina Mpango wa Kuanzisha Mwongozo wa Huduma kwa Waliopona Magonjwa ya Mlipuko hususan ugonjwa wa Marburg na Ebola,tiba kwa Mgonjwa ikiwemo Msongo wa Mawazo na Magonjwa mengine ya mwili pamoja na kuzuia Maambukizi.

Thank you for reading this post, don't forget to subscribe!

Akizungumza Mjini Biharamulo katika Maandalizi ya Mwongozo huo, Dkt. Joseph Hokororo kutoka Kitengo cha Uhakiki, Ubora wa Huduma za Afya, Wizara ya Afya amesema mwongozo huo utasaidia namna ya ufuatiliaji kwa Wagonjwa waliopona ugonjwa wa Marburg au Ebola ili kuondoa unyanyapaa katika Jamii.

“Tupo hapa leo kwa ajili ya kutengeneza Mwongozo kwa ajili ya kusadia ufuatiliaji kwa watu waliowahi kuumwa ugonjwa wa Marburg na Ebola na wamepona , na mwongozo huu utasaidia kufuatilia wanaporudi kwenye jamii na kuweza kuondoa unyanyapaa, na msongo wa mawazo” amesema.

Kwanini Mwongozo huu uwe kwa ugonjwa wa Marburg na Ebola?

Dkt. Hokororo amesema katika baadhi ya viungo vya binadamu huwa kunaendelea kuwa na vijidudu vinavyoweza kudumu kwa mwaka mmoja licha ya kupona ambavyo vinaweza kuleta tena Maambukizi kwenye jamii hivyo kupitia mwongozo huo mtu aliyepona atafuatiliwa kwa mwaka mmoja na kuweza kupatiwa huduma na isiwe chanzo cha kuleta maambukizi mengine.

“Katika mwili wa bindamu kuna baadhi ya viungo vya binadamu huwa kuna vijidudu(virusi) ambavyo vinaweza kuishi kwa mwaka mmoja , hivyo vikiendelea kuishi vinaweza kuleta maambukizi mengine kupitia mwongozo huu itasaidia kumfuatilia na kumsaidia mgonjwa ili asilete madhara tena kwenye jamii na pia kuondoa unyanyapaa “amefafanua .

Aidha, Dkt. Hokororo amesema Mwongozo huo utafuata utaalamu wote wa Kitaifa na Kimataifa na utakuwa na faida katika jamii ikiwa ni pamoja na utoaji wa huduma bora kwa wahusika na baada ya kukamilika zitafuata taratibu za kitaifa ikiwemo kusainiwa na Viongozi wa Taifa wenye dhamana ya kuusaini Mwongozo huo.