Home BUSINESS  RAIS SAMIA AELEZA NDOTO YAKE KUUREJESHA MKOA WA TANGA KUWA WA VIWANDA

 RAIS SAMIA AELEZA NDOTO YAKE KUUREJESHA MKOA WA TANGA KUWA WA VIWANDA

 

Thank you for reading this post, don't forget to subscribe!
TANGA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo ameeleza  ndoto yake ya kuurejesha Mkoa wa Tanga hadhi yake ya kuwa mkoa wa viwanda, akilenga  kufanya hivyo kwa kuweka sera thabiti na kujenga mazingira ya kuvutia uwezekaji. 

Rais Dkt. Samia ameeleza hayo leo mbele ya maelfu ya wananchi waliohudhuria mkutano  wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Mkwakwani.  

Vilevile, Rais Dkt. Samia ameeleza dhamira yake ya kuhakikisha Mkoa wa Tanga unakuwa pia mkoa wa utalii na kuwa unanufaika zaidi na fursa zitokanazo na fukwe, historia na  tamaduni mbalimbali ndani ya mkoa huo. 

Akizungumzia ziara yake ya wiki moja katika Mkoa wa Tanga, Rais Dkt. Samia ametoa rai  kwa wananchi kutumia ipasavyo fursa za maendeleo zitokanazo na miradi mbalimbali na  uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali ndani ya Mkoa wa Tanga.  

Aidha, ametoa rai kwa wananchi kuhakikisha vijana wanapata ujuzi na stadi stahiki  ikiwemo kupitia shule, vyuo vya VETA viliyojengwa katika kila wilaya, Chuo cha Mafunzo  ya Amali cha Mkoa na kampasi ya Chuo Kikuu Mzumbe kinachotarajiwa kujengwa katika  Wilaya ya Mkinga, ili waweze kunufaika zaidi na miradi mbalimbali inayofanyika katika  mkoa huo. 

Kwa upande mwingine, Rais Dkt. Samia amezungumzia changamoto ya viwanda na  mashamba yaliyobinafsishwa na Serikali kutoendelezwa kinyume na makubaliano ya  ubinafsishaji, hali inayowanyima wananchi fursa mbalimbali ikiwemo za uzalishaji, ajira na  masoko ya mazao yao. 

Hivyo, Rais Dkt. Samia amesema Serikali itapitia mikataba ya ubinafsishaji ya viwanda na  mashamba ambayo hayajaendelezwa na kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria kwa  lengo la kuhakikisha kuwa viwanda na mashamba husika yanawanufaisha wananchi. 

Kesho tarehe mosi Februari 2025, Rais Dkt. Samia anatarajia kuhitimisha ziara yake ya wiki  moja mkoani wa Tanga, ambapo pamoja na mambo mengine atafanya ziara kwenye  Bandari ya Tanga iliyofanyiwa maboresho makubwa na Serikali kwa lengo la kuimarisha  utendaji na uwezo wa bandari hiyo. 

Sharifa B. Nyanga 

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu