
Katika hotuba yake, Dkt. Kongela aliwapongeza wajumbe wa baraza kwa mijadala yenye tija, hususan kuhusu bajeti ya Shirika kwa mwaka 2025/26, ambayo inalenga kuboresha utendaji wa Shirika kupitia miradi mbalimbali ya ujenzi na ukarabati wa nyumba. Aliwahimiza wafanyakazi wa NHC kuendelea kuwa wabunifu, waaminifu, na kujituma katika majukumu yao, akisisitiza kuwa mshikamano na maadili bora ndio nguzo ya mafanikio ya Shirika.
Thank you for reading this post, don't forget to subscribe!Katika kuendeleza maendeleo, Dkt. Kongela alieleza kuwa Shirika limepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa miradi mikubwa kama awamu ya kwanza ya Samia Housing Scheme, ambayo inahusisha ujenzi wa nyumba 560 katika Kawe, Dar es Salaam, pamoja na majengo ya ofisi za Serikali katika Mji wa Serikali Mtumba. Alibainisha kuwa mafanikio haya yamewezeshwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, hususan katika kurahisisha upatikanaji wa fedha kwa miradi ya kimkakati ya ujenzi.
Akisisitiza umuhimu wa usimamizi thabiti wa rasilimali za Shirika, Dkt. Kongela alitoa wito kwa wafanyakazi kuhakikisha ukusanyaji wa madeni ya kodi ya pango unaimarishwa ili kuongeza mapato ya Shirika. Alihimiza kila mfanyakazi kufanya kazi kwa uwazi, bidii, na mshikamano, akisisitiza kuwa majungu na makundi hayana nafasi katika Shirika linalojizatiti kufanikisha malengo yake.
Mkutano huu umejadili masuala muhimu ya kimkakati kwa ajili ya maendeleo ya Shirika, ambapo wajumbe wametakiwa kuhakikisha kuwa NHC inaendelea kutoa gawio kwa Serikali, ambalo kwa mwaka huu linakadiriwa kufikia shilingi bilioni 6.5.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa amesisitiza dhamira yake ya kuongoza Shirika kwa weledi, uadilifu, na bidii ili kuhakikisha ongezeko la ufanisi na tija katika utoaji wa huduma bora za makazi nchini. Kwa msingi huo, NHC itaendelea kutekeleza yafuatayo:
Kuongeza Ufanisi – Kuboresha mifumo ya usimamizi wa miradi, rasilimali watu, na huduma kwa wateja ili kuongeza uzalishaji na kupunguza gharama zisizo za lazima.
Kufanya Kazi kwa Weledi – Kuhakikisha kuwa kila hatua inazingatia viwango vya kitaalamu na ubora wa hali ya juu.
Kujenga Uadilifu na Uwajibikaji – Kusimamia rasilimali kwa umakini, kuongeza uwazi na uwajibikaji wa wafanyakazi kwa maslahi ya umma.
Kuhamasisha Ubunifu na Ushirikiano – Kushirikiana na wadau wa sekta ya ujenzi, taasisi za kifedha, na wawekezaji ili kuongeza upatikanaji wa nyumba za gharama nafuu.
Kusimamia Miradi ya Kimkakati – Kutekeleza miradi mikubwa ya makazi na biashara katika mikoa mbalimbali ili kusaidia kupunguza uhaba wa makazi na kuchochea maendeleo ya miji.
Kwa kushikamana na maadili ya kazi, bidii, na mshikamano, wafanyakazi wa NHC wataendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha maendeleo endelevu ya sekta ya makazi nchini. Mkutano wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa NHC kwa mwaka 2025 sasa umefungwa rasmi.