Home LOCAL MKUTANO WA PILI WA BRELA NA WADAU, NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA...

MKUTANO WA PILI WA BRELA NA WADAU, NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA ASISITIZA MIFUMO ISOMANE 

Na: Neema Mathew, Dar-es-Salaam

Wakala wa usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Katika Mkutano wake wa pili na wadau wa mwaka 2024, Naibu Waziri wa viwanda na Biashara Mh.Exaud Kigahe amesisitiza taasisi hiyo na wadau wake kuendelea kuhakikisha kuwa mifumo inasomana.

Akizungumza wakati wa Mkutano huo mapema leo  Octoba, 25, 2024, jijini Dar-es-Salaam, Mh.Kigahe ameipongeza BRELA kwa mafanikio makubwa waliyoyafikia tangu kuanzishwa kwake na kuanzishwa mfumo wa digital ambapo ulianza mwaka 2018.

Amesema kwa Sasa taasisi hiyo imepiga hatua kubwa zaidi kwa kufanya mifumo inasomana kwa baadhi ya taasisi nyingine za kiserikali ikiwemo TRA,TIRA, NIDA na taasisi nyingine wanazofanya nazo kazi.
“Dhamira ya Rais wetu Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kuona mpaka Desemba 2024, kuhakikisha taasisi zote za Kiserikali mifumo inasomana ili kurahisisha huduma kwa haraka na kwa wakati, hivyo basi niwapongeze sana kwa hatua kubwa mliyopiga hii imeondoa hata wale vishoka ambao wafanyabiashara walikuwa wakiwalipa kiwango kikubwa Cha pesa kwa ajili ya kusajili lakini kumbe kiwango Cha pesa kinachotakiwa Katika usajili ni kidogo hivyo imerahisha sana kwa mfanyabiashara sehemu yoyote Ile ambayo yupo anaweza kusajili biashara yake na kuepukana na vishoka.
“Serikali ilifarijika sana na Taarifa ya maboresho ya mazingira ya biashara na uwekezaji ambao  BRELA kuweza kusajili Makampuni na Majina ya Biashara pamoja na kutoa Leseni za Biashara ndani ya siku moja, Hii ni hatua kubwa katika uboreshaji wa mazingira ya biashara na imetokana na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita kupitia Wizara na Taasisi zake katika kuboresha mazingira ya Biashara na Uwekezaji.
“Natoa rai kwa BRELA kuwa wasibweteke na maboresho haya ya kimfumo kwani Teknolojia inabadilika kila siku, hivyo muweke mkakati wa kuhakikisha mnakwenda sambamba na maboresho ya Kiteknolojia ili huduma yenu izidi kuwa bora na wezeshi kwa mnao wahudumia.
Wakati akimkaribisha Naibu Waziri wa viwanda na Biashara Mh.Kigahe, Mwenyekiti wa bodi Toka BRELA Pro.Neema Mori amesema Kauli mbiu Yao ya mwaka huu ni “Mifumo ya kitaasisi inayosomana na uwezeshaji  wa biashara nchini” hivyo basi watahakikisha mifumo yote inasomana ili huduma ziweze kuwafikia wadau.
Na kwa upande wake Godfrey Nyaisa
ambaye ni Afisa Mtendaji Mkuu BRELA
amesema kuwa  Tarehe 4 Januari, 2018, BRELA ilianza kutumia mfumo mpya wa Usajili kwa Njia ya Mtandao “Online Registration System- ORS”, mfumo huo unatoa huduma zote za sajili na za baada ya sajili “Registration and Post Registration” zikiwa ni pamoja na sajili za Makampuni, Majina ya Biashara, Alama za Biashara na Huduma, Hataza pamoja na Leseni za Viwanda. Kwa upande wa Leseni za Biashara za Kundi “A” zilizohamishiwa BRELA kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara pia zinatolewa kwa njia ya Mtandao kupitia Mfumo wa “Tanzania National Business Portal – TNBP”. Huduma hizi zimerahisisha sana wateja kupata huduma popote pale walipo, huduma nyingine zikiwa ni kwa siku moja tu.
“Kabla ya mifumo hii kuanza wateja walikuwa wanalazimika kutoka sehemu zote za nchi kuja kupata huduma Dar es Salaam. Huduma nyingine zilikuwa zinagharimu kiasi cha TZS 1,000 lakini wateja walilazimika kutoka Mbeya, Arusha, Mwanza, Rukwa na mikoa mengine kufuata huduma hii.
“Mfumo huu wa ORS umetimiza miaka sita sasa, ni dhairi teknolojia na baadhi ya sheria zimebadilika sana. Hivyo, sisi kama BRELA tulishaanza maboresho ya Mfumo huo kwa kuufanya uwe bora na rafiki zaidi na katika mfumo wa sasa kuna baadhi ya taarifa zinazolazimu kujazwa zaidi ya mara moja, kitu ambacho mfumo ungeweza kuvuta taarifa hizo bila kuhitaji kujazwa tena.
“Zoezi la maboresho lilishirikisha maoni ya wadau kwani wao ndiyo watumiaji wakubwa wa Mfumo huu. Nitumie fursa hii, kuwashukuru sana wadau wetu kwani wamekuwa mstari wa mbele kutoa maoni na michango pale tunapohitaji kutoka kwao, siyo kwenye mifumo tu hata kwenye maboresho ya sheria sita tunazozisimamia na BRELA. Pindi, Mfumo utakapokamilika tutawaita tena wadau wetu na kuwapitisha katika maeneo yote muhimu yaliyoboreshwa.
Maboresho haya yamezingatia uwepo wa huduma zingine, mfano upande wa Leseni za Biashara, BRELA inaendelea na mashauriano na mamlaka zingine ili kutumia mfumo mmoja wa Leseni za Biashara utakao kuwa na uwezo wa kutoa Leseni za Kundi “A” zinazotolewa na BRELA na Leseni za Kundi “B” zinazotolewa na Serikali za Mitaa “Local Government Authorities” bila kuathiri mapato ya halmashauri husika.
“Napongeza Wizara kwa  kusimamia kwa dhati majadiliano ya kuwa na mfumo mmoja wa utoaji Leseni za Biashara. Uanzishwaji wa mfumo huu mmoja wa Leseni utaisaidia sana Serikali kwenye takwimu pamoja na kuthibiti upotevu wa mapato kwa kuondoa leseni za kuandikwa kwa mikono,”amesema Mr.Nyaisa.
Previous articleBALOZI NCHIMBI AWAFARIJI MZEE MAKAMBA NA FAMILIA YA MWAMBI
Next articleBSS YAZINDULIWA ,SASA NI BONGO STAR SEARCH AFRIKA

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here