Home LOCAL RAIS MWINYI AZINDUA RIPOTI YA JIOLOJIA NA UTAFITI WA MADINI ZANZIBAR

RAIS MWINYI AZINDUA RIPOTI YA JIOLOJIA NA UTAFITI WA MADINI ZANZIBAR

*GST yakamilisha Utafiti wa Miamba, Udongo na Maji Zanzibar

*Waziri Mavunde: Ripoti ya Jiolojia Zanzibar itachochea uwekezaji mkubwa

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi amezindua Ripoti ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Zanzibar uliyofanyika kwa ushirikiano kati ya Wataalamu kutoka Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) na Wataalamu kutoka Wizara ya Maji, Nishati na Madini Zanzibar (WMNMZ).

Uzinduzi huo umefanyika leo Septemba 12, 2024 katika Hoteli ya Golden Tulip iliyopo Kisiwani Zanzibar ambapo Rais Mwinyi ametumia nafasi hiyo kuwapongeza wataalamu hao kwa kazi nzuri iliyofanyika ya kubainisha aina ya madini na mahali yaliyopo visiwani humo.

Aidha, Rais Mwinyi amesema Ripoti hiyo ya Jiolojia itatumika kwenye sekta mtambuka zikiwemo Madini, Nishati, Maji, Ujenzi, Kilimo, Elimu, Afya na Utalii ambazo ni muhimu katika ustawi wa jamii na uchumi wa Zanzibar.

Pia, Rais Mwinyi ameitaka Wizara ya Maji, Nishati na Madini ya Zanzibar kuhakikisha inaisambaza ripoti hiyo kwa taasisi zote zinazoguswa na tafiti hizo ili kuifanyia kazi kwa manufaa ya Taifa na kuongeza tija kwenye uchumi wa nchi.

Vilevile, Rais Mwinyi ameitaka Wizara ya Madini kupitia taasisi ya GST kudumisha mashirikiano yaliyopo katika Sekta ya Madini na kusisitiza kuendelea kufanya tafiti mbalimbali kwa lengo la kuendelea kugundua maeneo mapya yenye viashiria vya madini, fursa za utalii na maeneo yenye majanga ya asili nchini.

Pamoja na mambo mengine, Rais Mwinyi ametoa Vyeti kwa wataalamu walioshiriki kufanya tafiti na kuandaa ripoti hiyo kama pongezi na kumbukumbu kwa wataalamu hao.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde amesema utafiti uliyofanyika visiwani Zanzibar utapelekea uimarikaji wa uchumi katika visiwa hivyo na kubadirisha maisha ya watanzania wanaoishi visiwani humo.

Waziri Mavunde amesema matarajio ya matokeo ya utafiti huo yatatumika kuvutia uwekezaji mkubwa na kuchochea uchumi wa Taifa.

Naye, Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar Shaibu Kaduara amesema utafiti uliofanyika katika visiwa hivyo ni utafiti wa awali utakaohitaji kufanyika kwa utafiti wa kina ili kubaini kiwango cha Madini yaliyopo visiwani humo.

Awali, Mkurugenzi Idara ya Nishati na Madini, Mhadindisi Said Mdungi akitoa wasilisho la kitalaamu kwa niamba ya Timu nzima ya Watalaam alieleza Zanzibar kuwa Jiolojia ya Miamba tabaka ambapo alitaja aina za hiyo miamba, udongo na viashiria vya miamba yenye maji. Kwa upande wa madini amesema miongoni mwao ni Madini Tembo ( Heavy Mineral Sand aina ya ilmenite, titanium, zircon na magnetite) Madini Ujenzi, Chokaa na Silica. Aidha, mambo mengine yaliyoibuliwa ni vivutio mbalimbali vya jiolojia pamoja na maeneo yenye vihatarishi vya majanga ya asili ya jiolojia

Previous articleWAZIRI MKUU: SERIKALI YASAJILI MIRADI YA DOLA BILIONI 8.65 NDANI YA MWAKA MMOJA
Next articleASKARI UHIFADHI NGORONGORO KUWA NA MAHUSIANO MAZURI NA WANANCHI

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here