Home LOCAL MIKAKATI YA SERIKALI KULINDA RAIA DHIDI YA WANYAMAPOLI -WAZIRI CHANA

MIKAKATI YA SERIKALI KULINDA RAIA DHIDI YA WANYAMAPOLI -WAZIRI CHANA

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi, Dkt. Pindi Chana (Mb) amesema Serikali itaendelea kuweka mikakati madhubuti za kuwalinda wananchi dhidi ya wanyamapori wakali na waharibifu hususan tembo huku akisisitiza kuwa ni wajibu Serikali kuhakikisha usalama wa wananchi wake.

Ameyasema hayo leo Septemba 6, 2024 alipokutana na baadhi ya Madiwani wa Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Meatu Mkoani Simiyu, leo kwenye ukumbi mdogo wa Pius Msekwa, Bungeni jijini Dodoma.

Wakati umefika wa kuwalinda wananchi wetu na kuendelea kuchukua tahadhari za kutosha hasa kwenye maeneo ambayo ni korido za wanyamapori na nimezielekeza taasisi zetu kuweka vibao ili kuwataarifu wananchi wasipite katika maeneo hayo” amesema Mhe. Chana.

Aidha, amesema Wizara ya Maliasili na Utalii inatekeleza mikakati mbalimbali ya kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu kuhakikisha wananchi wanakuwa salama ikiwa ni pamoja na kuangalia namna ya kuwaelimisha wananchi kupanda mazao ambayo hayavutii tembo kama ufuta, kuvalisha tembo viongozi kola za kuonyesha kundi la tembo linaelekea wapi na kujenga vituo vya askari wanyamapori.

Naye, Mbunge wa Jimbo la Meatu, Mhe. Leah Komanya ameishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kazi nzuri ya uhifadhi na kupambana na changamoto ya tembo katika Wilaya ya Meatu kwa kuwapatia gari, pikipiki nne na kuwajengea kituo cha Askari Wanyamapori.

Awali, akiwasilisha taarifa ya Baraza la Madiwani, Diwani wa Kata ya Mwandoya, Mhe. Basu Kayungilo amesema kuwa kumekuwa na athari za wanyamapori wakali na waharibifu kwa wananchi wanaoishi katika vijiji vinavyopakana na Pori la Akiba Maswa na Jumuiya ya Wanyamapori Makao.

Mhe. Kayungilo ameongeza kuwa Baraza hilo liliazimia kuunda timu itakayoonana na Waziri wa Maliasili na Utalii kwa lengo la kupata muafaka wa changamoto hiyo ikiwemo utaratibu wa malipo ya kifuta jasho/machozi pamoja na mgawanyo wa asilimia 25 zinazotolewa kama rufaa ya vijiji vinavyopakana na hifadhi.

Kikao hicho kimehudhuriwa na baadhi ya watumishi waandamizi kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii wanaohusika na masuala ya wanyamapori.

Previous articleWAKANDARASI SKIMU YA MKOMBOZI WATAKIWA KUMALIZA UJENZI IFIKAPO OCTOBA
Next articleKIWANDA CHA MAFUTA YA ALIZETI KUNUFAISHA WAKULIMA DODOMA

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here