Home LOCAL KAMATI YA NISHATI NA MADINI YATAKA KUONGEZA KASI UJENZI WA JENGO MAKAO...

KAMATI YA NISHATI NA MADINI YATAKA KUONGEZA KASI UJENZI WA JENGO MAKAO MAKUU WIZARA YA MADINI

-Ujenzi wafikia asilimia 85

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imemtaka Mkandarasi wa Jengo la Makao Makuu ya Wizara ya Madini linalojengwa Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuongeza kasi ili kukamilisha Mradi huo kwa ubora na muda uliopangwa bila kuchelewa.

Agizo hilo limetolewa leo Septemba 04, 2024 Jijini Dodoma na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Dkt. Mathayo David wakati wa ziara ya Kamati hiyo kukagua maendeleo ya mradi huo.

Ameeleza kuwa kuchelewa kukamilika kwa jengo hilo kunaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa utendaji wa Wizara ya Madini, ambayo ni muhimu sana kwa ustawi wa sekta ya madini nchini.

Wote tunafahamu kuwa Wizara ya Madini ni nguzo kuu katika uchumi wa Tanzania kutokana na mchango wake mkubwa katika pato la taifa, Mkandarasi sisi kama Bunge tunachotaka kuona ni nyie kuongeza kasi ya ujenzi wa mradi huu na kuhakikisha unakamilika kwa wakati ili kuipa wizara uwezo wa kufanya kazi zake kwa ufanisi zaidi.” amesema Dkt. Mathayo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa amesema kuwa kukamilika kwa jengo la Makao Makuu hayo ya Wizara kutatusaidia kufanya shughuli za usimamizi wa Sekta ya Madini kwa ufanisi mkubwa kutoka katika eneo moja.

Sisi kama Wizara tunashukuru kwa ziara yenu hii Kamati ya Bunge, tunaamini itasaidia kuongezeka kwa kasi katika ukamilishaji wa mradi, lengo la Wizara ni kufanya shughuli zote katika eneo hili kwa watendaji na wafanyakazi wetu kukaa hapa (one stop center)” amesema Dkt. Kiruswa.

Naye, Mhandisi wa Mradi huo kutoka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mhandisi Remigius Kaijage amesema kuwa ujenzi wa mradi huo unaogharimu shilingi bilioni 23 umefikia asilimia 85 na tayari vifaa vyote vipo eneo la kazi na kwamba kwa kuzingatia ushauri wa kitaalam kutoka kwa Mshauri ambao ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) mradi huo utakamilishwa kwa ubora.

Previous articleBASHUNGWA ATOA ONYO KWA MAKAMPUNI YA UJENZI YANAYOBABAISHA WATEJA WAO.
Next articleMHE.CHALAMILA AMEPOKEA TAARIFA YA KAMATI ALIYOIUNDA YA    SOKO LA KARIAKOO

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here