Home BUSINESS MAKAMPUNI KUTOKA CHINA KUWEKEZA ZAIDI YA DOLLA MILLIONI 312 TANZANIA

MAKAMPUNI KUTOKA CHINA KUWEKEZA ZAIDI YA DOLLA MILLIONI 312 TANZANIA

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Sempeho Manongi (kushoto) akipokea zawadi kutoka kwa Kiongozi wa Ujumbe wa Wafanyabiashara kutoka Jimbo la Shangzhou Shen Don baada ya kufanyika kwa kikao kati ya menejimenti ya Shirika la Maendeleo la Taifa(NDC) na ugeni wa wafanyabiashara hao kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

UJUMBE wa wafanyabiashara na wawekezaji wakubwa kutoka Jimbo la Changzhou nchini China umeeleza kwamba umeridhia kufanya uwekezaji wa zaidi ya dola za Marekani milioni 312 sawa na zaidi ya Sh bilioni 800 katika maeneo ya nishati,afya,ujenzi, kilimo na vifaa vya uchakataji.

Pia, ujumbe huo umeonesha nia kushirikiana na kutafuta wawekezaji katika maeneo takribani nane ambayo ni viwanda vya kujenga viwanda vya kuzalisha na kufunga pawatila, kuzalisha vifaa vya trekta, kuzalisha majenereta na pampu za maji, kuzalisha vifaa tiba, viwanda vya bidhaa za umeme na paneli za kuhifadhi baridi.

Akizungumza Dar es Salaam leo Machi 27,2024 wakati wa kikao kati ya ujumbe huo na menejimenti ya Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), Mhandisi Anna Nyangasi kutoka kampuni ya Canopus Energy Solutions, amesema ujumbe huo wa watu 11 wakiwemo wafanyabiashara,Wawakilishi kutoka serikalini pamoja na ujumbe wa Chama cha Kikomunisti cha China(CPC)umewasili nchini baada ya mwaliko wa kampuni hiyo kwa kushirikiana na kampuni ya Amec Group.

“Baada ya kuwasili kwa ujumbe huo na kufanyika kwa mazungumzo yenye kulenga fursa za uwekezaji umekubali kuwekeza katika mashine za kilimo dola za Marekani milioni 24.5 sawa na Sh. bilioni 61.5, vifaa vya tiba dola za Marekani milioni sita sawa na Sh.bilioni 15.3 na vifaa vya umeme dola za Marekani milioni mbili sawa na Sh bilioni 5.13.

Mhandisi Nyangasi ametaja maeneo mengine waliyovutiwa nayo kiuwekezaji kuwa ni vifaa vya ujenzi ambako watawekeza dola za Marekani milioni 11.3 sawa na Sh.bilioni 28.2 na vifaa vya uchakataji wa mafuta watawekeza dola za Marekani milioni 43 sawa na Sh. bilioni 110.2.

Awali akizungumza baada ya kufanyika kwa majadiliano mbalimbali kati ya ugeni huo wa China na Maofisa wa Shirika la Maendeleo la Taifa(NDC) Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Sempeho Manongi amesema wamefurahishwa na ujio wa wafanyabiashara hao ambao tayari wameonesha nia ya kuwekeza nchini na wengine washabainisha maeneo wanayotaka kuwekeza.

Amefafanua kwamba iujumbe wa wafanyabiashara na wawekezaji hao unaotoka katika moja ya majimbo China yaliyoendelea katika viwanda huku akibainisha mbali ya kuja kuwekeza lakini watapata nafasi ya kubadilishana uzoefu katika sekta ya uwekezaji hasa kwa kuzingatia Tanzania Kuna maeneo mengi yenye fursa za uwekezaji.

Pia amesema katika mazungumzo yao wamebaini kuna maeneo yanayoshabihiana kwa pande zote mbili kwa ajili ya uwekezaji. Hivyo jopo hilo la watalaamu limekuja na kuonyesha nia ya kutaka kwekeza nchini Tanzania.

“Katika majadiliano yetu na ugeni huu Tanzania tumetaja fursa za uwekezaji ambazo China inaweza kuwekeza nchini yakiwemo ya kuongeza thamani kwa mazao ya kilimo, uzalishaji wa madini ya viwandani kama chuma na maeneo ya kujenga kituo maalumu cha nishati jadidifu.

Pia amesema maeneo mengine ni maeneo ya kongani za viwanda huku akifafanua NDC tayari wanayo maeneo kwa ajili ya uwekezaji huo ikiwemo Kilimanjaro, Tanga na Pwani na eneo la nishati jadidifu kama vile uzalishaji wa umeme wa jua na upepo.

Pamoja na mambo mengine NDC imetumia mkutano huo kuwasilisha mpango mkakati wake katika uzalishaji wa umeme unaotokana na nishati jadidifu hasa ya jua na upepo.

Amefafanua awamu ya kwanza itahusisha uzalishaji wa umeme wa upepo katika maeneo saba wa megawati 320 na wa jua katika maeneo 12 wa megawati 1,106.

Aidha amesema wafanyabiashara hao mbali ya kufanya kikao na NDC watapata fursa ya kwenda Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kwa lengo la kupata uelewa wa jinsi ya kufuata taratibu za uwekezaji nchini.

Wakati huo huo Kiongozi wa Ujumbe wa Wafanyabiashara kwa upande wa serikali ya Jimbo la Shangzhou, Shen Don amesema ameambatana na wafanyabiashara wakubwa katika jimbo hilo wakiwemo wakurugenzi wa kampuni kwa ajili ya kujifunza na kuangalia fursa za uwekezaji zilizopo Tanzania.

Mwisho.

Previous articleKUSUASUA UJENZI LAINI YA UMEME TABORA-URAMBO KWAMSIKITISHA DKT. BITEKO
Next articleBoT YAFUTURISHA WADAU WAKE DODOMA
Hughes Dugilo is a Writer, News Producer, Video-Photographer Journalist, and Video Editor experienced for 20 years now performing in News, Documentary, Advertisements and Television Programs. Aside from all above he own and operate his Blog known as Green Waves Media TZ since 2018.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here