Home LOCAL WCF YATOA KMPYUTA ZENYE THAMANI YA SH MILIONI TANO MAHAKAMA YA KAZI

WCF YATOA KMPYUTA ZENYE THAMANI YA SH MILIONI TANO MAHAKAMA YA KAZI

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina(kushoto) akipokea kompyuta mpakato kutoka kwa Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Ngowi(kulia) katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika leo tarehe 27 Julai, 2023 kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo, iliyopo jijini Dar es Salaam.Kushoto ni Afisa Mahusiano ya Umma, Bi. Agness Mbumilla.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina(kushoto) akipokea kompyuta ya mezani kutoka kwa Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF),Bw. Deo Ngowi(kulia) katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika leo tarehe 27 Julai, 2023 kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo, iliyopo jijini Dar es Salaam.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (kushoto) akimpatia kompyuta mpakato Afisa Ugavi Mwandamizi wa Mahakama hiyo. Leah Mvungi baada ya kukabidhiwa na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akitoa hotuba yake ya kushukuru msaada huo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama hiyo, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo (wa pili kushoto), Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Ngowi (kulia)na (kushoto) ni Afisa Mahusiano ya Umma wa WCF, Bi. Agness Mbumilla.

Na:: Magreth Kinabo na Mwanaidi  Msekwa  – Mahakama

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina leo tarehe 27 Julai 2023 amepokea msaada wa kompyuta na kompyuta mpakato vyenye thamani ya shilingi milioni tano kutoka katika Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF).

Msaada huo umetolewa na Afisa Sheria Mwandamizi wa WCF, Bw.  Deo Ngowi ambaye amesema anakabidhi vifaa hivyo, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa mfuko huo, kwa Jaji Mfawidhi huyo katika makabidhiano yaliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo, iliyopo jijini Dar es Salaam.

“Leo tumepokea kompyuta mpakato moja (laptop) na komputa ya mezani moja (desktop) kutoka kwa wadau wetu hawa muhimu, yaani Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF).

“Kwa niaba ya Mahakama, namshukuru sana Dkt. Mduma, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) pamoja na Menejimenti yake yote. Kipekee namshukuru sana Mzee Emmanuel Humba Mwenyekiti wa Bodi ya WCF na wajumbe wote wa Bodi kwa kuridhia ombi letu la kupatiwa vifaa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA),” amesisitiza.

Ombi hilo lilitolewa na Jaji huyo tarehe 25 Aprili, 2023 wakati alipofika ofisi za WCF, Dar es salaam kwa ajili ya kujitambulisha kwa uongozi.

Aidha Mhe. Jaji Dkt. Mlyambina ameongeza kwamba Dira ya Mahakama ya Tanzania ni kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa wakati na kwa wote. Hivyo Dira hiyo imewekwa vyema kwenye nguzo ya pili ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania wa Miaka Mitano wa awamu ya kwanza na pili kuanzia (2015/16 hadi 2020/2021 na 2021/22 mpaka 2024/25.

“Utekelezaji wa Dira ya utoaji haki unahitaji ushiriki mkubwa wa wadau kwa njia moja au nyingine. Komputa mpakato na komputa ya mezani tulizopokea leo zitaongeza ufanisi na kuboresha sana mchakato wa utoaji wa haki hapa Mahakamani na kumaliza kabisa mrundikano wa mashauri,” amebainisha.

Amefafanua kuwa Mahakama hiyo inalenga migogoro yote baina ya mwajiri na mwajiriwa isikae zaidi ya miezi mitatu tangu kufunguliwa kwake. Kwa kuwa kwa kufanya hivyo kutachangia kukua kwa uchumi wa watu  na Taifa kwa sababu  watatumia muda wao mwingi kwenye shughuli za uzalishaji badala ya kuzunguka kwenye vyumba vya Mahakama.

Mhe. Jaji Dkt. Mlyambina ameeleza hupokeaji wa vifaa hivyo ni jambo la kurahisisha na kuharakisha utoaji haki hasa kwa njia ya TEHAMA ni kubwa na ni la kimkakati endelevu.

Hivyo kwa niaba ya Mahakama, amemshukuru Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Menejimenti, Mwenyekiti wa Bodi ya mfuko huo, Mzee Emmanuel Humba na wajumbe wote kwa kuridhia ombi  hilo, la  kuunga mkono juhudi za Mahakama za kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa vitendea kazi kwa watumishi.

Aliihakikishia WCF, kuwa vifaa vya TEHAMA walivyovitoa vitatunzwa na kutumiwa vizuri kwa lengo lilokusudiwa. Na endapo tutapata vifaa vingine zaidi vitasaidia kuboresha huduma sehemu zingine zenye migogoro mingi ya kikazi.

Mfuko huo pia  mnamo tarehe 9 na 10, Juni 2023, kwa ruhusa ya Mhe. Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Ibrahim Hamis Juma kupitia kwa Mhe. Jaji Kiongozi Mustapher Mohamed Siyani, WCF waliandaa mafunzo kuhusu Sheria.

Mafunzo hayo yalifanyika kwa Wahe. Majaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Naibu Wasajili, Wasaidizi wa Sheria wa Majaji na Wasuluhishi/ Waamuzi kutoka Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) wa Mkoa wa Dar es Salaam na Wilaya ya Bagamoyo, Pwani, ambayo yamekuza weledi wa Maafisa wa Mahakama na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi katika ufanisi wa utatuzi wa migogoro ya kazi inayofikishwa mbele yao.

Kutokana na umuhimu wake aliiomba WCF kuendelea kutoa mafunzo kama hayo kwa Maafisa wengi wa Mahakama na CMA hususani katika Kanda zenye migogoro mingi ya kikazi ambazo ni Kanda za Arusha, Mwanza, Mbeya, Iringa, Tanga, Dodoma, Musoma na nyinginezo, kwani Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi ipo tayari kushirikiana nao ili kuhakikisha mafunzo yanafanyika kwenye Kanda zingine.

Previous articleWAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA NA MKEWE MARY WAKISALIMIANA NA PUTIN
Next articleHAKI YANGU FOUNDATION, SHY MC WATOA ELIMU YA HOMA YA INI KWA WANAFUNZI CHUO CHA UALIMU SHINYANGA
Hughes Dugilo is a Writer, News Producer, Video-Photographer Journalist, and Video Editor experienced for 20 years now performing in News, Documentary, Advertisements and Television Programs. Aside from all above he own and operate his Blog known as Green Waves Media TZ since 2018.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here