Home LOCAL WAZIRI MKUU: ANZISHENI MAJUKWAA YA KIUCHUMI

WAZIRI MKUU: ANZISHENI MAJUKWAA YA KIUCHUMI

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameagiza viongozi na watumishi katika balozi waendelee kufanya tathmini ya fursa za kiuchumi ambazo Tanzania inaweza kupata kutokana na ushirikiano wa kidiplomasia kwenye nchi walizopo.

Amesema ni vema balozi hizo zikaanzisha majukwaa ya kiuchumi yatakayowakutanisha wafanyabiashara na wawekezaji wa nchi hizo katika sekta mbalimbali za kiuchumi ikiwemo ardhi, madini, utalii, mawasiliano na biashara.

“Muwasihi wafanyabiashara na wawekezaji waje kuwekeza Tanzania na washirikiane na Watanzania kufungua makampuni, hii itatusaidia Watanzania kubadilishana uzoefu wa namna bora ya kuendesha biashara.”

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Ijumaa, Desemba 30, 2022) wakati akizungumza na watumishi wa ubalozi wa Tanzania ulioko jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Amesema watumishi wa balozi za Tanzania hawana budi kuandaa makubaliano baina ya Tanzania na nchi walizoko ambayo yataonesha nini kinatakiwa nchini humo na ambacho kinapatikana kwa wingi nyumbani Tanzania.

“Hapa kwenu, ubalozi unapaswa kutengeneza makubaliano maalum ya kibiashara miongoni mwa nchi hizi mbili na kubainisha aina ya bidhaa ambazo zinapatikana Tanzania kwa wingi na zinahitajika Afrika Kusini,” amesisitiza.

Aidha, Waziri Mkuu amesema ni vema pia ubalozi huo ukaendelea kuhamasisha watalii kutoka nchini humo kwa kubainisha vivituo vya utalii vilivyoko Tanzania ambavyo nchi hiyo haina huku akitolea mfano Mlima Kilimanjaro.

Awali, akitoa taarifa ya kiutendaji ya ubalozi huo, Kaimu Balozi Peter Shija alisema Tanzania inaweza kunufaika zaidi na fursa za biashara zilizopo nchini humo kwa kuuza mazao kama, mchele, maharage, korosho na mazao ya matunda.

Previous articleMAGAZETI YA LEO IJUMAA DISEMBA 30-2022
Next articleSAIDO, BOCCO WAPIGA HAT TRICK SIMBA IKIIPIGA 7-1 PRISON’S
Hughes Dugilo is a Writer, News Producer, Video-Photographer Journalist, and Video Editor experienced for 20 years now performing in News, Documentary, Advertisements and Television Programs. Aside from all above he own and operate his Blog known as Green Waves Media TZ since 2018.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here