Home LOCAL SHAKA: MAENDELEO, RAIS SAMIA NI KULWA NA DOTO

SHAKA: MAENDELEO, RAIS SAMIA NI KULWA NA DOTO

-Asisitiza ajenda ya maendeleo kwa wananchi ipo katika mikono salama, Watanzania waendelee kumuunga mkono

KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka, amesema Rais Samia Suluhu Hassan ni mwana maendeleo thabiti na mwana CCM kindakindaki ambaye amedhamiria kuleta maendeleo.

Shaka amesema kuwa Rais Samia ameonyesha kwa vitendo uthunutu wa hali ya juu kuleta maendeleo ya kweli kwa wananchi.

Ameyasema hayo leo Oktoba 16, 2022 alipokaribishwa kusalimia wananchi wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Taifa mjini Kibondo akiwa katika ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan mkoani Kigoma.

“Niwahakikishie wana Kigoma na niwahakikishie Watanzania, ajenda ya maendeleo kwa Rais Samia Suluhu Hassan ipo katika mikono salama. Maendeleo na Samia Suluhu Hassan ni kama kulwa na doto,” amesema.

Amesema Chama Cha Mapinduzi (CCM) kipaumbele chake cha kwanza ni maendeleo na hilo limedhihirishwa na mkataba ambao Rais Samia, wabunge na madiwani walikabidhiwa katika uchaguzi wa 2020.

”Tathimini ya kazi mnayoifanya ndio hii ambayo leo sisi kama Chama tumekuwa na wewe mguu kwa mguu, kuona namna gani ambavyo mmetekeleza yale ambayo tumewaahidi Watanzania. Ndugu Mwenyekiti kama ni duka sisi CCM ndio wamiliki wa duka hili…ninayo furaha kumwambia ndugu Samia Suluhu Hassan biashara mnaifanya vizuri sana kuwaletea maendeleo Watanzania

Kwa mujibu wa Shaka, CCM na wananchi ni mashuhuda wa kazi kubwa inayofanyika kila siku kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi.

“Leo hii wote tumeshuhudia wewe, timu yako na sisi CCM tumeshuhudia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025 ulivyofanyika kwa ufanisi mkubwa ndani ya Mkoa huu wa Kigoma.

“Tumeshuhudia utekelezaji wa Ibara ya 83 ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM, tuliahidi kuimarisha huduma za afya kwa kujenga majengo ya kisasa na kusimamia upatikanaji wa vifaa tiba, mmefanya kwa ufanisi mkubwa. Tumeshuhudia utekelezaji wa Ibara ya 100 inayohusu kuimarisha na kuhakikisha kwamba usaambazaji na upatikanaji wa maji safi na salama ndani ya Mkoa huu wa Kigoma,” amesema.

“Mheshimiwa Rais tukijumlisha yote kwa ufupi umetekeleza kwa vitendo Ibara ya 46 na 49 ya kuimarisha na kufungua uchumi wa Wana-Kigoma na mikoa ya jirani. Mheshimiwa Rais Mwenyezi Mungu akutunze ili Watanzania waendelee kunufaika.

AVIPONGEZA VYAMA VYA UPINZANI KUUNGANA NA RAIS SAMIA.

Aidha, Shaka amewashukuru viongozi wa vyama vya siasa vya upinzani walioshiriki mkutano huo ili kumuunga mkono Rais Samia.

“Tunawashukuru kwa kuja kuona mambo mazuri, karibuni tuungane pamoja tuijenge nchi yetu, nchi ni moja na taifa ni moja , Rais Samia ameanza vizuri kutuunganisha Watanzania mbali na imani zetu na itikadi zetu lakini Tanzania ni moja,” amesema.

Previous articleJOKATE ATOA MAELEKEZO KUIMARISHA STENDI YA MABASI YA MIKOA YA KUSINI
Next articleTANZANIA KUONDOKANA NA UPUNGUFU WA SUKARI 2023
Hughes Dugilo is a Writer, News Producer, Video-Photographer Journalist, and Video Editor experienced for 20 years now performing in News, Documentary, Advertisements and Television Programs. Aside from all above he own and operate his Blog known as Green Waves Media TZ since 2018.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here