Home LOCAL WANANCHI WA MADABA MKOANI RUVUMA WAMUANGUKIA RAIS SAMIA

WANANCHI WA MADABA MKOANI RUVUMA WAMUANGUKIA RAIS SAMIA


WANANCHI wa Kijiji cha Ndelenyuma Kata ya Mkongotema Halmashauri ya Madaba Mkoani Ruvuma  wamemuomba Rais Samia Hassan Suluhu kuilinda haki yao ya kuishi katika kijiji hicho ambayo pia walipewa na aliyekuwa rais wa awamu ya tano Hayati Dkt John Magufuli akiwa katika ziara ya kikazi mkoani.

Wamesema kuwa wamefikia hatua ya kumuomba rais Samia kutokana na baadhi ya viongozi kutaka kuwatoa kijijini hapo kwa kile walichodai wapo kwenye hifadhi licha ya kwamba kijiji kina usajili ambao ulitokana na kauli ya Hayati Dkt.Magufuli kuwakabidhi rasmi mwaka 2019 na ilipofika Agasti 9 mwaka huohuo walipata hati ya usajili wake.


Akizungumza kwaniaba ya wananchi wake Mwenyekiti wa Kijiji hicho cha Ndelenyuma Stanley Ngailo amesema kuwa wako katika stofahamu kubwa hadi sasa kutokana na kutakiwa kukihama kijiji hicho kwakile kinachodaiwa ni eneo la hifadhi jambo ambalo limeibua taharuki kwa wananchi.

”Tunamuomba sana sana Rais Samia Saluhu Hassan kutusaidia ili kuilinda haki yetu kwani kijiji hiki kinahati ya kusajiliwa ya Agasti 9 2019 baada ya Rais Hayati Dkt. Magufuli kutukabidhi rasmi Aprili 9, 2019”amesema Ngailo

Ngailo ameongeza kuwa wanapitia changamoto nyingi sana kijijini hapo kiasi kwamba yeye kama Mwenyekiti anapata  hofu ya usalama wake nakudai kuwa kuna watu wenye mamlaka wanasema eneo hilo ni hifadhi kitu ambacho wao kinawashangaza kwani wako kwenye eneo hilo kwa miaka mingi kabla hata ya uperesheni vijiji.

kwa upande wake Felix Lukas Mfunda ambaye ni Chifu wa kijiji hicho amesema kuwa amepata mateso makubwa ambayo yamempelekea kubaki masikini baada ya mali zake zote kuteketezwa kwa moto na watu ambao wanawataka kuondoka kwenye eneo hilo la kijiji na kudai hadi sasa amepewa kesi ambazo hazina hata ushahidi.

Amesema yeye alikuwa anaishi eneo la Mbunde ambalo lipo kijiji hicho cha Ndelenyuma na ndio ilikuwa himaya kubwa ya kichifu nakwamba akiwa katika shughuli zake siku moja walikuja watu na kumtaka aondoke kwenye eneo hilo huku wakiteketeza kila kitu kilichokuwepo hapo.

Ameongeza kuwa anamaumivu makubwa sana, na amebaki masikini mali zake zote zimeteketea kwa moto zikiwemo fedha tasilimu Milioni 85,trekta, machine za kusaga ,duka kubwa la huduma za kijamii na mambo yake ya kimila yote yaliteketea.

Amesema kuwa katika eneo lake hilo palikuwepo na kaya 75 pamoja na nyumba 300 ambazo zilikuwa ni za wananchi zote hizo zilitekezwa moto na mashamba ambayo yalikuwa na mazao yote yalichomwa moto hali ambayo imesababisha familia kutawanyika.

Amefafanua kuwa mateso wanayoyapata ni kwasababu ya watu wenye nguvu kutaka watoke kijijni hapo kwa madai kuwa wapo  maeneo ya hifadhi huku wengine wakisema maeneo hayo yana madini hivyo wanataka wao watolewe ili mambo mengine yaendelee kitu ambacho kinawashangaza kwasababu wao wamezaliwa maeneo hayo hadi kufikia uzee sasa hawajawahi kuona hifadhi yeyote.

Naye Mweyekiti wa wazee kijijini hapo Modestus Luoga amesema kuwa hajawahi kuona ushoroba kwenye eneo hilo kwani yeye amezaliwa hapo na maisha yake yote amekuwa hapo hivyo leo anashangaa anapoambiwa aondoke kwasababu maeneo hayo ni ya hifadhi.

Previous articleSIMAMIENI VIZURI FEDHA ZA HALMASHAURI-MAJALIWA
Next articleRAIS MHE. SAMIA SULUHU HASSAN AKUTANA NA VIONGOZI WA CHAMA CHA ACT WAZALENDO
Hughes Dugilo is a Writer, News Producer, Video-Photographer Journalist, and Video Editor experienced for 20 years now performing in News, Documentary, Advertisements and Television Programs. Aside from all above he own and operate his Blog known as Green Waves Media TZ since 2018.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here