Home BUSINESS SABABU ZA STAMICO KUWA KINARA MAONESHO YA SABASABA 2021

SABABU ZA STAMICO KUWA KINARA MAONESHO YA SABASABA 2021

Na: Hughes Dugilo, DAR ES SALAAM.

Maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa yaliyoanza Juni 28 mwaka huu na kufunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Isidor Mpango Julai 5, 2021 yamefikia tamati yake leo Julai 13,2021 katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere Dar es Salaam. Katika Maonesho hayo yaliyofanyika kwa zaidi ya siku 10 yaliyokuwa na Kauli mbiu ya Uchumi wa Viwanda Kwa Ajira na Biashara endelevu’ yamekamilika na yalikuwa na washiriki 3002 ambapo nchi 7 za kigeni zilishiriki yakiwemo makampuni 76.

 

Mnamo tarehe 5 Julai siku ya Jumatatu Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mpango alifika kuyafungua rasmi Maonesho hayo sambamba na kutoa zawadi mbalimbali kwa washindi watatu wa juu waliopata ushindi kwenye Maonesho. SHIRIKA la Madini la Taifa (STAMICO) liliibuka Kidedea na kupata ushindi wa jumla ikifuatiwa na Tume ya Sayansi (COSTECH) na ushindi wa tatu kuchukuliwa Benki Kuu ya Tanzania (BOT).

 

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt Venance Mwasse hakusita kuonesha furaha yake na kusema kuwa wanajisikia furaha kuchukua tuzo hiyo na kwani imewapa chachu ya kuendelea kuwa bora nyakati zote na kufanya kazi kwa bidii muda wote ili kukuletea Taifa la Tanzania mafanikio kwenye Sekta ya Madini. Jambo kubwa lililowavutia watu wengi kufika kwenye Banda la STAMICO ni ubunifu mkubwa waliofanya, muonekano na mpangilio vitu mbalimbali katika Banda, namna walivyojipanga kuwahudumia wananchi lakini zaidi ni mabalozi wa Mkaa Mbadala, Rafiki Briquette ambao ni Mamisi waliokuwepo Bandani hapo muda wote kwaajili ya uhamasishaji wa matumizi ya mkaa mbadala na kuwakaribisha wageni, ubunifu huo uliwafanya kuwa tofauti na wengine wakati wote wa Maonesho.

 

Mradi wa Mkaa Mbadala wa makaa ya mawe unaotarajiwa kuzalishwa kwaajili ya matumizi ya Majumbani nao umegusa watu wengi wakiwemo wageni mbalimbali waliofika STAMICO kujionea shughuli zao. Mhandisi Mtaalamu Uchenjuaji Mandini kutoka STAMICO Happy Mbenyange alifanya kazi nzuri ya kuuelezea na kuutangaza mkaa huo, ambapo alieleza kuwa mkaa huo ni rafiki na kwamba tayari kuna mtambo maalum ambao umeagizwa utakaoweza kutengeneza mkaa huo katika umbo la duara hivyo mara baada ya kuwasili kwa mtambo huo shughuli rasmi za uzalishaji zitaanza tayari kwaajili ya kuusambaza kwa wananchi kwa kutumia mawakala mbalimbali kwenye mikoa yote Nchini.

 

“STAMICO kwa kuunga juhudi za Serikali kupitia Kampeni Kabambe ya Usafi na Kuhifadhi Mazingira tumekuja na products mpya ya mkaa mbadala unaotumika kupikia majumbani, unaotokana na makaa ya mawe yanayochimbwa huko Kiwira. Mkaa wetu tunaupunguza nguvu ili kuweza kutumika nyumbani, haauna moshi, hauna majivu na sumu zote zimetolewa kwaajili ya matumizi ya nyumbani” Alisema Mhandisi Happy.

WAGENI MBALIMBALI WALIOTEMBELEA STAMICO (SABASABA).

katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Zanzibar Mhe. Juma Reli (kulia) akitia saini Kitabu cha wagaeni mara Baada ya kumaliza ziara yake fupi ya kutembelea Banda la STAMICO kwenye maonesho ya Sabasaba yanayoendelea Jijini Dar es Salaam.

Mwandisi mchenjuaji Madini wa Shirika la Madini la Taifa Happy Mbenyange (wa pili kushoto) akitoa maelezo jinsi ambavyo Shirika hilo lilivyojiandaa kutengeneza mkaa ambao utatuma majumbani kupikia kutoka katika makaa ya mawe ya kiwira kwa katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Zanzibar Mhe. Juma Reli (wa pili kulia) alipofika kwenye Banda la STAMICO lililopo ndani ya Banda la Wizara ya Madini kwenye Maonesho ya 45 ya Kimataifa ya Biashara yanayofanyika kwenye viwanja vya Sabasaba Jijini Dar es Salaam. (wa kwanza kushoto) ni Afisa Uhusiano wa STAMICO Bibiana Ndumbaro.  

Mnamo Julai 4,2021 katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Zanzibar Mhe. Juma Reli alifika kwenye Banda la STAMICO kuona na kujifunza jinsi ambavyo Mradi huo wa Mkaa Mbadala wa Makaa ya Mawe na kuufurahia. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Liberata Mulamula nae alipata nafasi ya kutembelea Banda hilo Julai 4,2021 na kuvutiwa Sana na Mradi huo wa mkaa mbadala, hivyo kuitaka STAMICO kujitangaza zaidi ili watanzania na wadau mbalimbali waweze kunufaika na mradi huo. 

WAZIRI wa  Mambo ya nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki liberata Mulamula (wa pili kulia)  mara baada ya kumaliza ziara yake katika Banda hilo.  

MABALOZI wa nchi mbalimbali wakafuatia kwenda kujionea Mradi huo, BALOZI wa uturuki nchini Tanzania Dkt. mehment Guluioliu. alionesha kuvutiwa zaidi na mradi huo na kusisitiza uwe endelevu.

BALOZI wa uturuki nchini Tanzania  Dkt. mehment Guluioliu akiweka saini kitabu maalum cha wageni katika Banda la STAMICO lililopo ndani ya Banda la Wizara ya Madini Maonesho ya Sabasaba Jijini Dar es Salaam.

“Mradi wa makaa ya mawe ni mradi mzuri na ni sahihi kwani pamoja na kuwa utafaa kwa matumizi ya majumbani lakini pia utaondoa uharibifu unaotokana na ukataji miti hivyo na badala yake watu watatumia nishati mbadala itokanayo na makaa ya mawe.” Alisema Dkt. Mehmet.

Florence Masuka (wa kwanza kulia)  Mwenyekiti Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Dar es Salaam akipata maelezo katika Banda la STAMICO kwenye Maonesho ya Sabasaba Jijini Dar es Salaam.

Kamati ya Utekelezaji wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT) kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salam nao walifika STAMICO kutembelea Banda hilo. Mjumbe wa Kamati ya Chama hicho (NEC) Angel Akilimali alisema sababu za kuamua kutembelea banda hilo la STAMICO pamoja na mambo mengine, Shirika hilo limekuwa likiendeleza wachimbaji wadogo wa madini na kuwajengea uwezo wa kuchimba madini katika mazingira salama yasiyo hatarishi kiafya.

“Tunawashukuru STAMICO kwa kupata fursa ya kutembelea hapa pamoja na mabanda mengine yaliyomo humu, tumekutana na wajasiriamali wanawake tumejifunza na kupata uzoefu wao katika shughuli wanazofanya zikiwemo katika sekta ya madini. Alisema.

Wageni hawakuishia hapo kwani hata Miss Tanzania 2020 Bi. Rose Manfere nae alijitokeza na kufika STAMICO na kuipongeza kwa kazi nzuri inayofanya kwa kipindi chote cha maonesho ya 77 katika kuelimisha umma hasa kuhusu uchakataji na uongezaji thamani katika Madini, matumizi ya mkaa mbadala wa Rafiki Briquettes akiweka wazi kufurahishwa kufika katika banda bora la STAMICO na kupata elimu juu ya shughuli mbalimbali zinazofanywa na STAMICO. Kwa ujumla hao ni baadhi tu ya wageni kati ya wengi waliopata nafasi ya kufika kwenye maonesho ya Sabasaba Mwaka huu na kutembelea Banda Kinara, na Mshindi wa Jumla la Shirika la Madini la Taifa (STAMICO). 

Ama kwa hakika Shirika hili linahitaji pongezi nyingi na kuungwa mkono kwenye kazi zao za kuliletea Taifa Maendeleo. Niwazi kuwa Mradi huo mpya wa Mkaa mbadala wa Makaa ya mawe, Rafiki Briquettes ni mkombozi kwa Mtanzania ikizingatiwa zaidi ya asilimia tisini (90%) ya Watanzania hutumia nishati ya mkaa kupikia hivyo mkaa huo mbadala unaenda kuleta ufumbuzi wa changamoto za kuharibika kwa Mazingira kunakotokana na ukataji wa miti ya kuchomea mkaa.

Previous articleHISTORIA YA NCHI YETU HAIWEZI KUKAMILIKA BILA YA HAYATI MZEE MKAPA’-RAIS SAMIA
Next articleHABARI ZA MAGAZETI LEO ALHAMISI JULAI 15-2021

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here