Home BUSINESS PROFESA MKUMBO ATANGAZA NEEMA YA UJIO WA KIWANDA CHA BIA CHA TBL...

PROFESA MKUMBO ATANGAZA NEEMA YA UJIO WA KIWANDA CHA BIA CHA TBL JIJINI DODOMAWANANCHI WAASWA KUCHANGAMKIA FURSA

DODOMA

Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) inatarajia kujenga   Kiwanda kipya cha kuzalisha bia jijini Dodoma. 
 
Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Profesa Kitila Mkumbo alipofanya ziara katika Kiwanda cha TBL jijini Dar es Salaam kujionea utendaji kazi na changamoto zilizopo. 

Akitangaza neema ya ujio wa kiwanda cha bia cha TBL jijini Dodoma, Profesa Mkumbo amesema  ujenzi wa kiwanda hicho ni matokeo ya uboreshaji na uwekaji wa mazingira bora ya uwekezaji nchini ili kuvutia wawekezaji wadogo na wakubwa kutoka sehemu mbalimbali duniani kuja kuwekeza nchini.

Akitoa maelezo ya ujenzi wa kiwanda hicho unaotarajiwa kuanza Mwezi Julai mwaka 2022 na kutarajiwa kukamilika mwaka 2023, Prof Mkumbo ametoa rai kwa wakulima wa shayiri nchini kuongeza uzalishaji kwa kuwa soko la uhakika lipo na linazidi kutanuka. 

“Nawapongeza TBL kwa nia pamoja na kuanza mchakato wa kufungua kiwanda chao kingine jijini Dodoma ambacho ujenzi wake utaanza Mwezi Julai, 2022 na kukamilika mwaka 2023 na kuanza uzalishaji” alisema Prof. Mkumbo 

Mbali na pongezi hizo, Prof. Mkumbo amewataka TBL kubadili mtazamo wa kibiashara kwa kuwa na mawazo ya kujipanua kibiashara na kushindana kikanda na si kuwaza soko la Tanzania pekee jambo ambalo linaenda sambamba na msisitizo wa Serikali kwamba, bidhaa zetu ziuzwe nje zikiwa bidhaa kamili au bidhaa zilizoongezwa thamani na kuacha utamaduni wa kuuza malighafi. 

Akitolea ufafanuzi kuhusu suala la kodi ya bia kushushwa, Waziri Mkumbo amebainisha kuwa, punguzo hilo la kodi ni kwa zile bia ambazo zimezalishwa kwa kutumia shayiri ya Tanzania kwa asilimia 100 na si bia zote na kuongeza kuwa hatua hiyo inalenga katika kuchochea kilimo cha shayiri nchini na kuhamasisha uanzishwaji wa viwanda vya bia nchini katika kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira nyingi. 

Akitoa neno la shukrani, Meneja wa Kodi kutoka Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), Bw. Avito Swai ameishukuru Serikali kwa hatua ya kupunguza kodi kwenye viwanda vya kuzalisha bia jambo ambalo limepunguza gharama za uendeshaji na kuwezesha uanzishaji wa  viwanda  vingine  zaidi.

Bw. Swai ametumia fursa hiyo pia kuwasilisha changamoto ya gharama za Mfumo wa Stika za Kielektroniki (ETS) huku akiomba Serikali kuwapunguzia gharama hizo.

Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia vinywaji vyake ni miongoni mwa walipa kodi wakubwa hapa nchini na kutajwa kuwa na mchango mkubwa katika Serikali na uchumi wa nchi kwa ujumla ambapo pia ni miongoni mwa wachangiaji wakubwa wa pato la Taifa huku ikiongoza kwa kutoa ajira nyingi kutoka mwanzo hadi mwisho wa mnyororo wa thamani wa uzalishaji wa bia zake na hivyo kuonekana kuwa na mchango mkubwa katika maisha ya watu hapa nchini na uchumi wa taifa kwa ujumla.
Previous articleHABARI KUU ZILIZOPO MAGAZETINI IJUMAA YA LEO JULAI 23-2021
Next articleKUKABILIANA NA SUALA LA LISHE SHINYANGA.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here