Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, ametoa salamu za Sikukuu ya Pasaka katika Tamasha la Mtoko wa Pasaka lililoandaliwa na Wasanii wa Muziki wa Injili nchini.
Hafla hiyo iliyofanyika Jumapili tarehe 20 Aprili 2025 katika Ukumbi wa Super Dome, Masaki, jijini Dar es Salaam, ilihusisha wasanii nguli wa muziki huo, wakiongozwa na Christina Shusho, kupitia taasisi yake ya Relax East Africa Limited.
Akizungumza katika tukio hilo, Dkt. Nchimbi alisisitiza umuhimu wa kudumisha mshikamano, amani, na upendo miongoni mwa Watanzania. Alihimiza jamii kuendeleza maadili mema na kuimarisha mshikamano wa kitaifa kama msingi wa maendeleo endelevu.
Aidha, aliwapongeza waandaaji wa hafla hiyo kwa kubuni na kutekeleza wazo la kuwaunganisha watu katika kusherehekea Pasaka, akibainisha kuwa matukio kama hayo yanachangia kuijenga jamii yenye mshikamano na matumaini kwa ajili ya mstakabali mwema wa taifa.